Tuesday , 10th Nov , 2015

Mshambuliaji wa zamani wa Tanzania na Simba SC, Alhaj Abdallah Seif ‘King Kibaden’ ameteuliwa kuwa kocha wa timu ya Tanzania Bara, itakayoshiriki michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge 2015 nchini Ethiopia.

Kibaden ambaye pia ni kocha wa klabu ya JKT Ruvu ya ligi kuu, amepewa jukumu la kuteua benchi zima la ufundi la Taifa Stars, lakini zaidi atachukua watu kutoka benchi la Taifa Stars ambapo ingizo jipya linatarajiwa kuwa mtu mmoja pekee, ambaye ni kocha msaidizi lakini meneja, kocha wa makipa, mtunza vifaa na daktari watakuwa wale wale wa Taifa Stars.

Kocha mkuu wa sasa wa Taifa Stars, Charles Boniface Mkwasa atakwenda Ethiopia kama mshauri wa ufundi wa vikosi vyote, Bara na Zanzibar, ambayo itakuwa chini kocha msaidizi wa Taifa Stars, Hemed Morocco.

Michuano hiyo ambayo itaanza Novemba 21 hadi Desemba 6 mwaka huu ambapo Tanzania Bara imepangwa kundi A pamoja na wenyeji Ethiopia, Zambia na Somalia, wakati Kundi B lina timu za Uganda, Burundi na Djibouti huku Kundi C likiundwa na Sudan Kusini, Sudan, Zanzibar na Rwanda.