Wednesday , 22nd Jun , 2016

Beki hodari wa kulia wa Klabu ya Yanga Juma Abdul Mnyamani ameanza mazoezi rasmi mara baada ya kuendelea vizuri kwa hali ya kifundo cha mguu wake kilichopelekea kushindwa kucheza dhidi ya Mo Bejaia.

Juma amesema, ameanza mazoezi ikiwa ni sehemu ya kujipanga kwa ajili ya kukabiliana dhidi ya TP Mazembe Juni 28 mwaka huu.

Juma amesema, anaamini atapambana na anaamini mchezo utakuwa mgumu kwani TP Mazembe ni timu nzuri kwa Afrika lakini wapizani wao pia wanajua wanakuja Tanzania kukutana na timu nzuri.

Juma amesema, katika mchezo wa awali ambao hakuweza kuwa na kikosi chake dhidi ya Mo Bejaia kilichoathiriki kikosi ni hali ya hewa pamoja na mfumo ambao ulibadilika kutokana na kukosekana kwa baadhi ya wachezaji.

Juma amewataka mashabiki kujitokeza kwa wingi katikia mchezo dhidi ya TP Mazembe ili kuwapa hamasa wachezaji na kuhakikisha wanaibuka na ushindi katika mchezo huo.

Kwa upande wa meneja wa Juma Abdul, Zumo Jumbe amesema, walichelewa tiba hapo awali na hivi sasa wameshaanza tiba na anaendelea kumsimamia katika mazoezi ili kuhakikisha hai yake inaendelea kuimarika.

Zumo amesema, anaamini Juma atakuwa vizuri na iwapo atapata nafasi katika kikosi cha awali dhidi ya TP Mazembe ataonyesha uwezo wake kwani kwa sasa hali yake inaendelea kuwa nzuri.

Juma Abdul anatarajia kuungana na kikosi cha Yanga kitakaporejea kutoka nchini Uturuki Juni 25 kilipoweka kambi ya maandalizi ya mchezo wake dhidi ya TP Mazembe.