Wednesday , 6th Jan , 2016

Uongozi wa klabu ya Borussia Dortmund ya Ujerumani umesema nyota wao Piere Emereck Aubameyang hakuhudhulia mazoezi ya jana ya klabu yao kutokana na masuala yake binafsi ambayo hayahusiani na suala la kutaka kuhama.

Mshambuliaji wa kimataifa wa Gabon na klabu ya Borussia Dortmund Piere Emereck Aubameyang akishangilia moja ya goli alilofunga katika mechi ya ligi kuu nchini Ujerumani.

Msemaji wa klabu hiyo ametoa taarifa kupitia akaunti ya twita ya timu ambayo imeweka wazi kuwa nyota huyo atakuwepo leo mazoezini kwa ajili ya kuendelea na maandalizi ya mechi za ligi zinazofuata.

Ingawa taarifa ndani ya klabu zinauhakikishia uma kuwa nyota huyo bado ataendelea kuwepo kwenye viunga vya Signa Iduna Park upo uvumi kutoka nchini Ujerumani na Uingereza unaomhusisha mshambuliaji huyo kuwa huenda akatua katika klabu ya Arsenal.

Mshambuliaji huyo raia wa Gabon ambaye mkataba wake unamalizika mwaka 2020 amekuwa kwenye kiwango bora msimu huu na sasa ndiye kinara kwa ufungaji katika Bundesilga akifunga mabao 17 na 27 kwenye mashindano yote.