Wednesday , 6th Jul , 2016

Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhandisi Gerson Lwenge amewashauri wananchi kuchangia gharama za maji ikiwa pamoja na ulipaji wa bili za maji kwa wakati ili waweze kupata huduma endelevu za maji safi na salama nchini.

Mhandisi Gerson ameyasema hayo alipotembelea banda la maji la Shirika la Maji Safi na Maji Taka jijini Dar es Salaam-DAWASCO katika maonesho ya Sabasaba yanayoendelea jijini humo ambapo amesema endapo wananchi watalipa bili za maji kwa wakati watawawezesha watoa huduma wa Dawasco kutoa huduma bora za maji na kwa wakati muafaka kwa wateja wake.

Mhandisi Gerson amebainisha kuwa wizara yake haitavumilia kuona watu wachache wanahujumu miundombinu ya kusafirisha maji na kupelekea wananchi kuwa na uhaba wa maji safi na salama.

Naye Afisa Mtendaji wa DAWASCO, Crispin Luhemeja, ametoa wito kwa watanzania ama wateja wote wa Dawasco wenye uwezo mdogo wa kuunganisha maji kutembelea ofisi za Dawasco ili waweze kusaini mkataba wa maunganisho mapya ya maji kwa gharama nafuu na kulipa kidogo kidogo.