Saturday , 16th Jan , 2016

Watu wawili wamekamatwa wakiwa na meno ya tembo yenye thamani ya shilingi milioni 54.8 mkoani Manyara

Askari wa Hifadhi ya Taifa ya Manyara Mkoani Arusha, kwa kushirikiana na jeshi la polisi wamefanikiwa kuwakamata Jamali Saidi na Damasi Komba wakiwa na Meno ya Tembo yenye thamani ya shilingi milioni 54 na laki nane.

Watuhumiwa hao wawili wamekamatwa wakiwa katika harakati za kutafuta wateja wa men ohayo ambapo waliwekewa mtego baada ya taarifa zao kunaswa na kitengo cha Intelijensia cha TANAPA na ndipo wakakamatwa.

Akiongea mara baada ya kufanikiwa kuwakamatwa watuhumiwa hao jana mkurugenzi mkuu wa mamlaka ya hifadhi za taifa [TANAPA] Alan Kijazi, amesema kazi hiyo nzuri ni muendelezo wa jitihada zinazofanywa na askari wa mamlaka hiyo.

Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Manyara, Domisiani Njau amesema hivi sasa wanajishughulisha na ulinzi wa hifadhi hiyo usiku na mchana kuhakikisha wanadhibiti wizi wa nyara za serikali.

Watuhumiwa hao wanatarajia kufikisha mahakamani kujibu mashtaka kwa kukutwa na nyara za serikali.