Monday , 15th Feb , 2016

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora Angella Kairuki ametangaza kuwachukulia hatua watumishi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini wanaotajwa kufanya vitendo ambavyo ni kinyume na maadili ya utumishi.

Akizungumza leo jijini Dar es salaam wakati akifungua mkutano wa TAKUKURU, Mhe. Kairuki amesema watendaji hao wana wajibu wa kuhakikisha taasisi hiyo inafanya kazi kwa kuzingatia uweledi, kufanya uchunguzi kwa wakati ili kuwafikisha watuhumiwa mahakamani.

Mhe.Kairuki amesema anafahamu kumekuwa na Minong'ono ya watendaji wa mikoa kulalamikiwa kwa kujihusisha na ubadhirifu wa mali ya umma, uchunguzi unaendelea na watakaobainika hatua zitachukuliwa za kuwawajibishwa na sheria kuchukua mkondo wake.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Valentino Mlowola amesema atahakikisha watendaji walio chini yake wanatimiza adhma ya serikali ya kuwasimamia watumishi wa umma, kufichua ubadhirifu unaofanywa na watendaji wa taasisi za serikali ili kuhakikisha miradi ya serikali inatekelezwa kadri ilivyo kusudiwa.

Mlowola amesema watendaji wa mikoa wasisite kuwachukulia hatua maafisa ardhi wanaotajwa kuhusika na rushwa na kusababisha migogoro ya wakulima na wafugaji inayoongezeka kila kukicha.