Saturday , 6th Dec , 2014

Baadhi ya wanaume wameanza kuripoti matukio ya kunyanyaswa na wake zao katika Madawati ya Jinsia mkoani Ruvuma

Matukio ya wanaume kunyanyaswa na kufanyiwa ukatili na wake zao ikiwemo kumwagiwa maji ya moto na hata wengine kukatwa viungo vyao yameshika kasi mkoani Ruvuma ambapo baadhi ya wanaume wameanza kuripoti matukio ya kunyanyaswa na wake zao katika madawati ya Jinsia.

Hayo yameelezwa na wanaharakati wa haki za binadamu kwenye kongamano la maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia lililoandaliwa na shirika la kuhudumia watoto yatima Ruvuma (ROA) la Mkoani Ruvuma.

Akifungua kongamano hilo mkuu wa wilaya ya Songea Bw. Joseph Mkirikiti amewataka wanawake kuwafundisha mabinti kuheshimu ndoa zao ili kukomesha unyanyasaji huo.