Thursday , 25th Jun , 2015

Jeshi la polisi mkoani Kagera limefanikiwa kukamata waganga wa jadi wawili wanaosadikiwa kuwa ni vinara wa kuchochea mauaji ya watu wanao chinjwa na kuondolewa koromeo

Waganga wa jadi waliokamatwa

Jeshi la polisi mkoani Kagera limefanikiwa kukamata waganga wa jadi wawili wanaosadikiwa kuwa ni vinara wa kuchochea mauaji ya watu wanao chinjwa na kuondolewa koromeo huku wakiwa na tunguli za aina mbalimbali pamoja na jambia moja ambalo linasadikiwa kuwa limekuwa likitumika kufanya mauaji hayo.

Akiongea mara baada ya kuwakamata waganga hao wa jadi kamishina msaidizi wa jeshi la polisi mkoani Kagera ACP Gilles Mloto amesema watuhimiwa hao walikamatwa wilayani Misenyi wakiwa na jambia moja pamoja na dawa za kila aina ambazo mara nyingi huwapa waharifu kama ngao ya kujilinda wakati wa kufanya uharifu na kwamba waganga hao walikamatwa mara baada ya wananchi kuwavamia na kutaka kuwashambulia ndipo jeshi hilo lilipo ingilia kati na kuwakamata na sasa wamefikishwa katika kituo cha polisi mjini Bukoba kwaajili ya upelelezi zaidi.

Kamishina msaidizi wa jeshi la polisi mkoani kagera acp Gilles Mloto ameongeza kwa kusema kuwa hivi karibu yamelipotiwa matukio ya mauaji ya watu watatu katika kata ya gela wilayani misenyi ambapo ametoa wito kwa wananchi kutoa ushirikiano wa hali ya juu ili kwa pamoja waweze kufanika kumata mtandao mzima wa waharifu wanao chinja watu na kuondoka na baadhi ya viungo vyao.

Ikumbukwe kwamba vitendo vya mauaji mkoani Kagera vimekuja kwa kasi tangu mwezi Agost mwaka jana ambapo hali hiyo bado imeendelea kuleta hofu kubwa kwa wakazi wa mkoa wa Kagera ambapo sasa wengi wao wamekuwa wakiahirisha shuguli zao na kuamua kurudi mapema majumbani wakihofia kuuawa.