Wednesday , 8th Jul , 2015

Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Chiku Gallawa amewataka wakazi wa Mkoa wa huo kutumia fursa ya ugeni mkubwa wa mkutano Mkuu wa CCM kufanya biashara na kujiongezea kipato.

Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Chiku Gallawa.

Gallawa ametoa kauli hiyo leo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na ugeni wa wajumbe wa mkutano mkuu wa CCM ambapo unatarajiwa kufanyika juma hili kwa ajili ya kumpata mgombea urais atakayekiwakilisha chama hicho kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Octoba mwaka huu.

Amewataka wananchi wa mkoa huo na wajasiriamali kuhakikisha kuwa wanaitumia fursa hii kwa ajili ya kutoa huduma nzuri kwa wageni watakaokuja kwenye mkutano huo ili kujiongezea kipato na kuboresha biashara zao.

Hata hivyo Jana kamanda wa polisi mkoa wa Dodoma, David Misime amewataka wageni wasiokuwa na shughuli za lazima za kuja kufanya mkoani hapa wasije mpaka mkutano mkuu wa CCM utakapomalizika kwa ajili ya kuepuka usumbufu utakaojitokeza wa kukosa mahali za kulala kutokana na kwamba nyumba zote za wageni zimeshajaa.