Tuesday , 20th Jan , 2015

BAADHI ya wafanyabiashara na wakulima wa zao la viazi mkoani Njombe wamelalamikia ubadhilifu unaofanywa na kamati ya kuzuia rumbesa, kisha kufukuzwa kwa wateja wao ambao walikuwa wakitegemea kuwapata kwa msimu huu wa viazi.

Mkuu wa Wilaya ya Njombe Sarah Dumba.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na waandishi wa habari mkoani Njombe wafanyabiashara hao wamesema kuwa wamekuwa wakitozwa fedha zisizo na kiwango maalumu kama faini ya kujaza viazi katika magunia maarufu kama rumbesa, ambapo wamekuwa wakifanya hivyo kwa lengo la kushindania soko la zao hilo jijini Dar es Salaam.

Mmoja wa wafanyabiashara wa viazi mkoani Njombe Ephraim Haule amesema kuwa mshono ambao unatakiwa kushonwa katika magunia ya viazi wafanyabiashara kutoka jijini Dar es Salaam wanakataa kununua viazi hivyo kwa kuwa watashindwa kuviuza wakifika sokoni.

Naye Charles Sanga amesema kuwa wamekuwa wakikabiliana na kukimbiwa na wateja wafikapo katika soko la viazi kutokana na viazi vyao kuwa katika magunia yaliyo na ujazo mdogo kulinganisha na viazi kutoka mikoa ya Mbeya Iringa, Arusha na nchini Kenya ambavyo huwa na rumbesa.

Hata hivyo Mmoja wa wafanyabiashara aliye bahatika kukutana na tume ya ofisi ya mkuu wa wilaya Kanoti Bosco, amesema kuwa alitozwa faini ya zaidi shilingi 520,000 na kukatiwa stakabadhi ya shilingi 420,000 na kudaiwa kuwa shilingi laki moja ni kwaajili ya mafuta ya kuwafuata huko waliko katika vituo ya kukagulia magunia.

Amesema kuwa serikali kwa kufanya hivyo inawadidimiza wafanya biashara na wakulima kwa kuwa zao hilo halitunziki gharani na kuwa wamekuwa wakikutana na changamoto ya kuhalibikiwa kwa zao hilo kutokana na kukosa wateja huku likiwa tayali limesha tayarishwa kuingia sokoni.

Amesema kuwa wafanyabiashara wao hawana shida na kuto weka rumbesa shida ipo katika ushindani wa soko ambapo wao wakitoka shamba wanakutana na rumbesa na kuwa kiazi kunacho toka nchini Kenya kinajazwa nusu ya gunia kama rumbesa na inaitwa Obama.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Njombe Sarah Dumba amesema kuwa timu hiyo ni yeye ameiunda baada ya kuona wananchi wanakandamizwa na rumbesa kwakuwa ujazo huo una kiuka sheria ya vipimo ambapo inatakiwa mazao yoyote ya chakula yanatakiwa kuuzwa yakiwa katika vipimo vya mizani.

Amesema kuwa katika msafara wa mamba na kenge wamo kwa maana kuwa huenda kuna rushwa ikawepo katika tume aliyoiunda ambapo katika tume hiyo kuna mtendaji wa kata husika kilipo kituo cha ukaguzi na kuwa amewapa vitambulisho ili kutambulika na kujitenga na wahalifu ambao wanaweza kutumia zoezi hilo vibaya.