Friday , 5th Feb , 2016

Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limesema lipo kwenye mchakato wa ujenzi wa mradi wa usambazaji wa gesi asilia kwa ajili ya matumizi ya majumbani, viwandani na kwenye magari katika mikoa ya Lindi na Mtwara.

Mojawapo ya Mitambo inayotumika kusambaza gesi nchini Tanzania

Hayo yamezungumzwa jana mkoani Mtwara na meneja wa biashara ya gesi wa shirika hilo, Emmanuel Gilbert, baada ya kumalizika kwa semina ya siku moja ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari wa Mtwara juu ya uelewa wa sekta ya mafuta na gesi iliyoandaliwa na shirika hilo.

Amesema, mradi huo ambao kuanza kwake kunategemea na upatikanaji wa fedha, mtandao wake wa kutandaza mabomba utakuwa na urefu wa Km 17 kwa mkoa wa Mtwara ambapo unatarajiwa kuunganisha nyumba 11,000 na magari 4,000 ambayo yatakuwa na yana uwezo wa kuamua kutumia nishati ya gesi au mafuta, na Km 11 kwa mkoa wa Lindi.

Amewataka wananchi wa mikoa hiyo kuunga mkono mradi huo ambao ukikamilika utaokoa gharama za matumizi ya pesa kwa kiasi kikubwa ambacho wananchi wanatumia sasa katika manunuzi ya gesi kupitia mitungi na mafuta kwenye magari yao.