Wednesday , 27th Apr , 2016

Serikali ya Tanzania imesema itawasilisha muswada wa sheria katika bunge utakaohakikisha kuwa watoto wote wanaosoma shule za msingi na sekondari hawatasitisha masomo yao kutokana na ndoa za utotoni.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe,

Hayo yamesemwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe, leo bungeni wakati akijibu swali la Mbunge wa Ileje Mhe. Janeth Mbene aliyetaka kujua ni lini serikali itafanya marekebisho wa sheria ya ndoa nchini.

Dkt. Mwakyembe amesema kuwa mswada huo pia utaleta mabadiliko katika sheria ya elimu ambapo itafanya watoto wote wa shule za msingi na sekondari waweze kufaidi matunda ya sera ya elimu bure kwa wote hususani kwa watoto wa kike.

Aidha ameongeza kuwa Wizara pamoja na tume ya kurekebisha sheria imepanga kulifanya zoezi la ukusanyaji wa maoni kuhusu sheria ya ndoa na sheria nyingine za wanawake kwa kuwafikia wanawake wengi zaidi kwa kutumia mfumo wa White paper.

Dkt. Mwakyembe amesema kuwa kutokana na mchakato wa kuundwa tume ya mabadiliko ya Katiba mpya, mchakato wa kufanya marekebisho ya sheria ya ndoa na mapendekezo ya kutungwa kwa sheria mpya ya mirathi na urithi ulisitishwa kwa muda ili kupisha ukusanyani wa maoni ya katiba mpya.

Waziri huyo wa katiba ameongeza kuwa baada ya tume ya mabadiliko ya katiba kukamilisha kazi yake imebainika kuwa maoni ya wananchi hayakujielekeza kwenye maudhia ya sheria ya ndoa na sheria ya mirathi ambapo amesema serikali imeanza mchakato wa kuendelea na taratibu za kutungwa kwa sheria hizo.

Sauti ya Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe, akiongelea sheria ya ndoa za utotoni