Tuesday , 18th Aug , 2015

Serikali imeanza kuwanoa wataalamu wa TEHAMA na maofisa wake wa idara mbalimbali, ili kuweza kuunganisha mitandao yote ya TEHAMA kwa ajili ya kukomesha taarifa za ubadhirifu wa fedha za umma na ucheleweshaji wa taarifa kwa wananchi.

Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais , Menejimenti ya Umma Bwana Hab Mkwizu (katikati) akizungumza na wanahabari

Akizungumza leo Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Habib Mkwizu, alipokuwa kwenye ufunguzi wa Kongamano la kwanza la serikali Mtandao la siku nne, linalofanyika Jijini humo.

Amesema wamekutanisha maafisa TEHAMA, Mipango, Habari, Utawala na Rasilimali watu ili wafundishwe jinsi ya kuunganisha mitandao yote kuwa mmoja serikalini.

Amesema kuwa kwa kuunganisha mitandao serikali itasaidia kutoa huduma bora kwa wananchi kwa kutoa taarifa muhimu kila ngazi kwa wakati mwananchi anapohitaji.

Mkwizu amesema pia serikali itaimarisha usalama wa taarifa zake na raia wake katika karne ya sayansi na teknolojia, kwa kuongeza uwezo wa serikali kupambana na majanga kwa kutumia teknolojia ya TEHAMA na itasaidia kutengeneza mfumo imara ndani ya serikali.

Akitoa mfano amesema kama sasa wananchi wanapata huduma safi shirika la TANESCO, kupitia ulipaji wa bili za LUKU kwa mtandao na Mamlaka ya Maji Safi na Taka, nao wanatoa huduma zao kwa mtandao na bili wananchi wanalipa huko, hivyo ni hatua za kupongezwa, japo mwisho wa siku wote wanatakiwa kuunganisha mitandao hiyo kuwa mmoja.

Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha (RAS), Adoh Mapunda amesema ni muhimu miundombinu yote ya mitandao ikapita katika mfumo mmoja ili kukomesha ubadhirifu na kurahisisha huduma bora kwa wananchi.

Amesema katika kongamano hilo watakuwa na wataalamu watakaotoa mafunzo ya kuunganisha mitandao serikalini kutoka Singapore Dk. Rajendra Kumar na mwingine toka nchini India, ambao wamepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa serikali mtandao duniani na mfano wa kuigwa duniani.