Monday , 4th May , 2015

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii nchini Dk. Seif Rashid amesema kuwa tafiti zilizofanywa katika nchi 72 zimeonesha kwamba upatikanaji wa huduma muafaka za ukunga umewezesha kupunguza kiwango cha vifo vya akina mama vinavyotokana na uzazi.

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii nchini Tanzania Dkt. Seif Rashid.

Dk. Seif ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati akizungumzia mpango mkakati wa kuongeza kasi ya kupunguza vifo vya mama na mtoto hapa nchini na kuongeza kuwa vifo hivyo vimepungua kwa wastani wa asilimia 3 kwa mwaka kuanzia mwaka 1990.

Dk. Seif ameongeza kuwa wizara itaweza kufika malengo ya maendeleo ya milenia namba 4 na 5 yanayohusu kuboresha afya ya mama kwa kupunguza vifo vya wanawake vinavyotokana na uzazi kwa robo tatu na kuweza kufikia wakina mama 193 kwa kila vizazi hadi laki moja pamoja na serikali kuongeza juhudi za kukabiliana na vifo hivyo.

Wakati huo huo, Shirika la viwango Tanzania TBS pamoja na shirika la viwango la Zanzibar ZBS leo wamesaini makubaliano ya ushirikiano ili kuongeza uwezo wa taasisi hizo katika kudhibiti viwango nchini.

Makubaliano hayo yamefanyika jijini Dar es Salaam leo kati ya waziri wa viwanda na biashara Dkt. Abdalah Kigoda pamoja na waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko wa Zanzibar Mh. Nassoro Mazrui, ushirikiano huo utasaidia kuhakikisha kuwa bidhaa zote zinazotoka na kuingia Zanzibar na Tanzania bara zinakuwa na ubora sawa unaokubalika kimataifa.

Aidha makubaliano hayo pia yatasaidia kuondoa mianya yote ya kupenya kwa bidhaa hafifu hasa katika mipaka ya nchi ambayo ni changamoto kwa mashirika ya TBS na ZBS, ushirikiano huo utakuwa katika maeneo ya kiufundi, mafunzo, kubadilisha wafanyakazi pamoja na taarifa nyingine.