Wednesday , 19th Aug , 2015

Watumishi wa serikali wametakiwa kutumia teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kuwahudumia wananchi ili kuondoa adha ya upatikanaji wa huduma hizo ambazo hulazimika kuzifuata kwenye ofisi za serikali.

Mkurugenzi wa TEHAMA Ofisi ya Rais-Utumishi Bw.Priscus Kiwango.

Njia hiyo ya mtandao inatajwa kuwa njia rahisi na ya haraka yenye ufanisi mkubwa inayopunguza suala la ucheleweshaji wa huduma muhimu za kijamii kama vile maji na umeme ambavyo vimekuwa vikilipwa kwa njia ya mtandao wa simu bila kumlazimisha mtumiaji kufika ofisi zinazotoa huduma hizo.

Akizungumza katika kongamano la siku nne 4 la masuala ya matumizi ya mtandao katika kuwahudumia wananchi, katibu tawala mkoa wa Arusha Ado Mapunda amesema kuwa kukua kwa mtandao kumerahisisha upatikanaji wa huduma hizo hivyo ofisi za serikali zinapaswa kutumia mitandao ili kuwafikia wananchi kwa muda mfupi na kupunguza msongamano katika ofisi za serikali.

Mtendaji Mkuu wa serikali Mtandao maarufu kama (e- government) Dr. Jabir Bakari ametoa wito kwa mashirika ya umma kuhakikisha kuwa yanasimika na kuboresha mifumo ya TEHAMA ili iweze kuwahudumia wananchi kwa urahisi zaid.

Kaimu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hab Mkwizu amesema kuwa licha ya huduma ya mtandao kusaidia wananchi bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo Kukosekana kwa usimamizi thabiti wa mfumo huo ili kuulinda dhidi ya watu wanaofanya udanganyifu kwa njia ya mtandao.

Kukua kwa teknolojia Tanzania na duniani kwa ujumla kumeifanya dunia kuwa kwenye kiganja hivyo wananchi kupata huduma muhimu kupitia simu ya kiganjani, mapinduzi haya yakisimamiwa vizuri yanaweza kuleta tija na ufanisi mzuri kwa manufaa ya watanzania wengi.