Friday , 23rd Jan , 2015

JESHI la polisi wilayani Kahama mkoani Shinyanga linamsaka afisa mtendaji wa kata ya Nyandekwa katika halmashauri ya mji wa Kahama Makoye Kintoki kwa tuhuma za kutoweka na fedha za mfuko wa jimbo zinazosaidia kusukuma maendeleo ya wananchi.

Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga Justus Kamugisha

Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga Bw. Justus Kamugisha amewaambia waandishi wa Habari kuwa Kintoki amelalamikiwa na mwajili wake halmashauri ya mji wa Kahama kutoweka na kiasi cha shilingi 1.7 milioni zilizokuwa zimetolewa na mbunge wa jimbo la Kahama Mhe. James Lembeli kwa ajili ya ujenzi wa gati la maji.

Amesema awali mtuhumiwa huyo alikuwa afisa mtendaji wa kata ya Malunga ambapo mbunge Lembeli alimkabidhi kwenye mkutano wa hadhara kiasi cha shilingi Milioni 2.0 kwa ajili ya ujenzi wa gati hilo mwanzoni mwa mwaka huu lakini mpaka sasa kazi hiyo haijafanyika na kutoweka nazo ingawa ukaguzi wa hesabu za ndani unaonyesha fedha alizotoweka nazo ni shilingi Milioni 1.7.

Kufuatia hali hiyo kamanda kamgisha amesema tayari halmashauri imemfungulia mashtaka katika kituo cha polisi Kahama mjini na kuwa jeshi lake linamsaka popote pale alipo ili kumfikisha mahakamani kujibu tuhuma hizo.

Kwa upande wake mkurugenzi wa halmashauri ya mji wa Kahama Bw. Felix Kimario pamoja na kukiri kumfungulia mashtaka Afisa mtendaji huyo amesema tayari ameshamwandikia barua ya utoro kazini baada ya kutoweka kwenye kituo chake cha kazi kwa muda mrefu bila taarifa.

Amesema pamoja na barua hiyo maandalizi ya kumfukuza kazi kwa utoro kazini taratibu zake za kikazi zinaendelea kufanyika huku akikili Afisa huyo kutoweka na fedha hizo za mradi wa maji kwa wananchi wa kata ya Malunga.