Tuesday , 8th Dec , 2015

Mtanzania Rachel Nungu ametajwa kuwa miongoni mwa vijana 60 ambao wanatarajiwa kupewa tuzo za viongozi wa kipekee kutoka nchi za jumuiya ya madola, ambayo itakabidhiwa nna Malkia Elizabeth.

Rachel Nungu ambaye ana umri wa miaka 27, ameteuliwa kushinda tuzo hizo baada ya kutambulika kwa kazi yake ya kutibu watoto waliozaliwa na ulemavu wa kupinda miguu, unaojulikana kwa jina la Club foot.

Akiongelea tatizo hilo kwa watoto ambalo ndio limemfanya ajulikane na ulimwengu, Rachel amesema watoto wengi ambao wamekuwa wakizaliwa na tatizo hilo wamekuwa wakifichwa kwenye jamii, lakini anajivunia kuifanya kazi hiyo na hatimaye kuchaguliwa kwenye tuzo hizo.

“Watoto ambao wanazaliwa na club foot mara nyingi wanafichwa, ni muhimu nimejenga uhusiano mzuri na viongozi wa jamii kwa lengo la kueneza mwamko na matibabu yake, tumefanikiwa kuanzisha kliniki katika mikoa tofauti na kutoa mafunzo kwa wahudumu, mpaka sasa tumekwisha saidia watoto zaidi ya 100, ninajivunia kuwa miongoni mwa mpango wa Malkia wa viongozi vijana”, alisema rachel.

Tuzo hizo ambazo zilianzishwa mwaka 2014, zitatolewa jijini London na mwenyewe Malkia Elizabeth mwaka 2016, ikiwa ni miongoni mwa mpango wa Malkia kwa viongozi vijana, ili kusherehekea mafanikio ya vijana walionyesha kupiga hatua na kubadilisha maisha ya wengine.