Wednesday , 23rd Mar , 2016

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka, ameagiza kukamatwa kwa meneja wa Mamlaka ya Maji safi mjini Maswa Jeriamia Lema kwa tuhuma mbalimbali ikiwemo utata wa gharama za chujio la Maji pamoja na kusambaza maji bila kuyatibu kwa kuyawekea dawa.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka

Mtaka ametoa agizo hilo mara baada ya meneja huyo kueleza kuwa ujenzi wa chujio hilo unatarajia kugharimu bilioni 7 huku mkandarasi akisema kuwa gharama halisi ni bilioni 3 na milioni 300.

Hatua hiyo imekuja baada ya ziara ya Mkuu huyo wa Mkoa wa Simuyu ambae aliongozana na Mkuu wa Wilaya ya Maswa Bi. Rosemary Kigirini, ambae ndie alieanza kuagiza Meneja huyo wa Mamlaka ya maji kukamatwa kutokana na kuonekana kuna ubadhirifu katika Ujenzi huo.

Katika kusisitiza kukamatwa kwa Meneja huyo baada ya Mkuu huyo wa Mkoa kufanya mahojiano na mkandarasi wa mradi ndipo alipagiza vyombo husika ikiwemo takukuru viweze kuchukua hatua zaidi katika jambo hilo.