Monday , 7th Dec , 2015

Serikali wilayani Chato mkoani Geita imepiga marufuku usambazaji na uuzwaji wa mifuko ya plastiki huku wafanyabiashara wenye maduka wakiamriwa kuiteketeza kwa moto kabla zoezi la kuwakamata na kuwafikisha mahakamani halijaanza.

Mkuu wa wilaya ya Chato,Shaaban Ntarambe

Amri hiyo imetolewa na Mkuu wa wilaya ya Chato,Shaaban Ntarambe,wakati akizungumza na wafanyabiashara kuhusiana na uimalishwaji wa zoezi la usafi wa mazingira.

Ntarambe amesema serikali imeamua kupiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki kwa kuwa imekuwa ni kichocheo cha uchafuzi wa mazingira na kwamba wafanyabiashara hao wanapaswa kuuza na kusambaza mifuko ya karatasi ambayo ni rahisi zaidi kuoza baada ya kumalizika matumizi yake.

Amesema agizo hilo linaanza kufanya kazi kuanzia leo na kwamba halitakuwa na faini kwa mfanyabiashara atakaye kamatwa akiuza bidhaa hiyo, na badala yake atafikishwa mahakamani kwa kuvunja Sheria.

Akizungumza na East Africa Radio,muda mchache baada ya kumalizika kikao hicho,mmoja wa wafanyabiashara wilayani hapa,Focus Manoni,amelalamikia agizo hilo na kudai linalenga kuwafirisi kwa kuwa baadhi yao bado wanamzigo mkubwa ambao waliununua kabla ya kutolewa kwa agizo hilo.

Kwa upande wake katibu wa wafanyabiashara wilayani hapa Rai Ntigwanamba, kushangazwa na agizo hilo huku ikipendekeza kufungwa viwanda vyote vinavyodhalisha bidhaa hizo badala ya kuwaamuru wafanyabiashara wa maduka kuteketeza mifuko hiyo.