Thursday , 4th Feb , 2016

Mke wa Rais wa Tanzania, Mama Janeth Magufuli ameziomba taasisi za serikali na binafsi kushirikiana katika kutatua changamoto zinazovikabili vituo na makazi ya wazee na walemavu wasiojiweza nchini Tanzania.

Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akihutubia wakaazi wa Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu cha Nunge, Kigamboni, jijini Dar es salaam alikotembelea

Hayo amesema jana wakati alipotembelea kituo cha makazi ya wazee na watu wenye ulemavu wasiojiweza cha Nunge, Kigamboni Jijijini Dar es Salaam ambapo alitumia fursa hiyo kuwakabidhi zawadi ikiwemo kilo elfu 3 za unga, kilo elfu 3 za mchele na kilo 1,200 za maharage.

Mama Janeth amezitaja baadhi ya changamoto zinazowakabili wazee hao ni pamoja na uchakavu wa miundombinu, uhaba wa rasilimali fedha na watu, pamoja na maslahi duni ya watoa huduma, upungufu wa vitendea kazi na huduma za jamii, pamoja na suala la uvamizi wa eneo la kituo.

Katika hotuba yake Mama Janeth ameahidi kushirikiana na wadau wote ili kuzitafutia ufumbuzi huku akimtaka mkuu wa wilaya ya Temeke kushughulikia tatizo la uvamizi wa ardhi katika eneo la wazee hao.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Temeke Bi Sophia Mjema amesema kuwa suala la uvamizi huo linashughulikiwa na tayari waziri mwenye dhamana ameshafika katika eneo hilo na kusema hatua zaidi zitachukuliwa.

Aidha mkuu huyo wa wilaya ametoa wito kwa wananchi wote nchini kuwatunza wazee ambao wanaishi katika mazingira magumu kwani wazee ni watu muhimu katika taifa lolote duniani

Mwenyekiti wa kituo cha makazi ya wazee na watu wenye ulemavu wasiojiweza, Nunge Kigamboni Mzee Anthony Kikongoti amemshukuru mke wa Rais Mama Janeth Magufuli kwa kuwakumbuka wazee hao ikiwa ni mara yake ya kwanza tangu Rais Magufuli aingie madarakani kutembelewa na kiongozi huyo wa ngazi ya juu