Tuesday , 29th Dec , 2015

Idara ya mahakama inahitaji zaidi ya Shilingi Bil.1.8 ili iweze kuwahamisha watumishi wa ngazi mbalimbali katika idara hiyo hapa nchini wapatao mia moja tisini na mbili waliokaa kwenye kituo kimoja cha kufanyia kazi kwa muda mrefu.

Jaji Mkuu, Othman Chande

Hayo yameelezwa na Jaji Mkuu, Othman Chande wakati akizungumza na watumishi wa idara ya mahakama katika mkoa wa Kagera ambako yuko kwa ziara ya siku mbili yenye lengo la kufuatilia utendaji wa kazi wa watumishi wa idara hiyo, amesema idara hiyo inashindwa kuwahamisha watumishi waliokaa sehemu moja kwa muda mrefu kutokana na ufinyu wa bajeti.

Aidha, Jaji huyo mkuu amezitaka mahakama zote nchini kufungua dawati la malalamiko litakalowapa fursa kuelezea kero mbalimbali wanazokumbana nazo mahakamani, pia amewataka watendaji wa mahakama kufupisha muda wa kutoa huduma kwa wananchi.

Kwa upande wake, Seif Kijita ambaye ni Kaimu msajili wa mahakama kuu kanda ya Bukoba amesema kuwa mahakama hiyo inaendelea kufanya jitihada kubwa za kupunguza mlundikano wa mashauri yanayoletwa katika mahakama hiyo, akitoa takwimu amesema mahakama kuu katika kanda hiyo kuanzia mwaka 2013 imepunguza idadi kubwa ya mlundikano wa kesi katika mahakama hiyo.