Friday , 9th Sep , 2016

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amezitaka nchi za Sudan Kusini na Burundi kudumisha amani kwa ajili ya maendeleo ya wananchi na jumuiya kwa ujumla.

Wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wakiimba wimbo wa Jumuiya hiyo wakiongozwa na Mwenyekiti wa sasa wa Jumuiya hiyo Rais wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli

Akitoa taarifa ya kikao cha dharura mara baada ya viongozi hao wa EAC kukutana jana Jijini Dar es Salaam Rais Dkt. Magufuli ametoa wito kwa nchi hizo zenye migogoro na machafuko kukaa pamoja kukubalina ili kudumisha amani katika mataifa hayo.

Dkt. Magufuli ametumia fursa hiyo kuitaka nchi ya Sudani kusini kuzitaka pande zinazopingana kuweka silaha chini kwa ajili ya majadiliano ili kuepusha vifo zaidi vinavyotokana na mgogoro huo uliosababisha vita katika nchi hiyo.

Aidha Rais Magufuli amesema kuwa taarifa ya mpatanishi wa mgogoro wa Burundi, Mhe. Benjamin Mkapa imetoa mapendekezo kadhaa ambayo yatasaidia kumaliza mgogoro huo ambao nao umesababisha wakimbizi wengi kukimbilia nchi nyingine za afrika mashariki.