Tuesday , 25th Nov , 2014

Mbunge wa jimbo la Kawe (CHADEMA) Halima Mdee amesema kuwa mfumo dume uliopo hapa nchini utaondolewa na wanawake wenyewe endapo watajiamini na kuondoa woga katika kutimiza malengo yao waliyojiwekea maishani hasa katika suala la uongozi.

Mbunge wa jimbo la Kawe,na Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema, Halima Mdee.

Mdee ametoa kauli hiyo jana wakati akizungumza na wanafunzi wa kike kutoka katika halmashauri ya Wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma ambao wako kwenye mradi wa kujengewa uwezo wa uongozi ujulikanayo kama "Haki yangu Sauti Yangu" mradi unaofadhiliwa na shirika lisilo la kiserikali la Woman Wake Up (WOWAP) lililopo Mkoani Dodoma.

Amesema kuwa kama wanawake hawataweza kusimama na kuuondoa mfumo dume uliopo hapa nchini hakuna mtu mwingine atakayeuondoa kikubwa ni kuamua na kujiamini kuwa wanaweza.

Aidha amewasihi wanawake nchini kumtanguliza Mungu katika kila hatua ya mafanikio yao wanayoipitia kwani bila Mungu hakuna watakachoweza kufanya.

Kwa upande wake mratibu wa mradi huo kutoka shirika la Wowap, Luhaga Mkunja alisema mradi huo ni mahususi kwa ajili ya kuwajengea uwezo wanafunzi wa kike ambao hata wakimaliza masomo yao wanaweza kuja kuwa viongozi wazuri katika jamii wanayoishi.