Thursday , 24th Mar , 2016

Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali - PAC imemuagiza Mhasibu Mkuu wa Serikali Bw. Francis Mwakapalila kuwasiliana na taasisi sita za serikali, kwa lengo la kukutana na kamati hiyo ili kupata hali halisi ya deni la taifa.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali PIC, Mbunge wa Sumbawanga Mjini, Aesh Hilary (katikati).

Lengo ni kuhakikisha kuwa kamati hiyo inaishauri vema serikali juu ya hatua zinazopaswa kuchukuliwa kupunguza deni hilo na ikiwezekana kuzuia mianya inayosababisha deni la taifa kuongezeka kwa haraka.

Pasipo kutaja kiasi halisi cha deni hilo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mbunge wa Sumbawanga Mjini, Mh. Aesh Hilary, amesema taasisi hizo ndizo zinazohusika na usimamizi wa moja kwa moja wa deni la taifa na kwamba ni vema bunge likapata picha halisi ya deni la taifa kwa sasa na hivyo kutoa ushauri wake.

Awali kabla ya agizo hilo, wajumbe wa kamati hiyo walikuwa na hoja mbali mbali mojawapo ikiwa ni suala la malipo ya pensheni kwa wastaafu ambapo mbunge wa Viti Maalumu mkoa wa Tabora Bi. Munde Tambwe amemtaka Mhasubu Mkuu wa Serikali kushughulikia usumbufu mkubwa wanaopata wastaafu wakati wanapofuatilia mafao yao serikalini.

Bw. Mwakapalila kwa upande wake amekiri kuwepo kwa usumbufu katika utaratibu wa kudai mafao na kuahidi kushughulikia mapungufu hayo huku akiwataka waajiri pamoja na maofisa masurufu kuandaa taarifa za wastaafu mapema ili kuiwezesha serikali kulipa mafao kwa wakati.