Wednesday , 1st Jul , 2015

Hifadhi ya taifa ya Ruaha mkoani imetumia zaidi ya shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa miradi ya ujirani mwema lengo likiwa ni kuimarisha mahusiano baina ya hifadhi hiyo na vijiji vinavyozunguka hifadhi.

Mkuu wa mkoa wa Iringa Bi. Amina Masenza.

Akitoa taarifa ya shirika hilo wakati wa kukabidhi Bweni la wasichana katika shule ya sekondari ya William Lukuvi iliyopo Pawaga Muhifadhi mkuu wa hifadhi ya taifa ya Ruaha Dkt. Christopher Timbuka ametaja miradi iliyotekelezwa kuwa ni pamoja na ya maji ujenzi wa madarasa miradi ya uhifadhi afya pamoja na matumizi bora ya ardhi.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Iringa Bi. Amina Masenza amewataka wanavijiji kushirikiana kikamilifu na shirika hilo katika kuhifadhi maliasili za taifa ili ziwe endelevu na kuendelea kuwapa faida wananchi hao na taifa kwa ujumla.

Diwani wa kata ya Ilolo mpya Bw. Fundi Mihayo akimuomba mkuu huyo wa mkoa kusaidia kusuluhisha mgogoro wa kimaslahi unaikabili jumuiya ya matumizi bora ya mali hai Idodi na pawaga (MBOMIPA) kwani kusambaratika kwa jumuiya hiyo kutasababisha ongezeko la ujangili katika hifadhi ya taifa ya Ruaha.

Bweni hilo la wasichana limejengwa kwa ushirikiano wa wananchi wa kata ya Ilolo mpya na hifadhi ya taifa ya Ruaha kwa thamani ya zaidi ya shilingi milioni 200 huku hifadhi ya taifa ya Ruaha ikichangia asilimia sabini na wananchi na wadau wengine asilimia 30 ambapo bweni hilo litakuwa mkombozi kwa wasichana wa shule hiyo ambao bweni lao liliungua na kuteketea kwa moto hivi karibuni hali iliyosababisha wakose mahali pa kulala.