Wednesday , 7th Jan , 2015

Waziri wa ujenzi, Mh. Dk. John Magufuli ameitaka ofisi ya wakala wa ufundi na umeme (TEMESA), kuboresha maslahi ya watumishi wa vivuko ili kuepukana na wizi wa mafuta yanayotumika katika kuendeshea mitambo pamoja na vivuko hapa nchini.

Waziri wa ujenzi, Mh. Dk. John Magufuli

Dkt. Magufuli amemuagiza mtendaji mkuu wa TEMESA mhandisi Marcelin Magessa, kuzingatia ushauri huo wa kuwaboreshea watumishi wake maslahi wakati alipokuwa akizindua mfumo mpya wa tiketi za eletroniki katika kivuko cha Kigongo - Busisi mkoani Mwanza.

Aidha Mh. Magufuli ameiagiza TEMESA kubadilisha muda wa kufanya kazi wa vivuko nchini toka saa 18 za awali hadi saa 24 ili kutoa huduma kwa wananchi wanaohitaji usafiri huo wakati wote.

Amesema serikali inafikiria mpango wa kujenga daraja katika kivuko hicho kutoka Kigongo wilayani Misungwi hadi Busisi wilaya ya Sengerema na kuwataka watendaji wa wakala wa barabara nchini Tanroads na TEMESA mkoani Mwanza kufanya upembuzi yakinifu katika bajeti ya mwaka wa fedha ujao.

Naye mtendaji mkuu wa TEMESA, mhandisi Marcellin Magesa amesema mfumo huo mpya wa ukatishaji tiketi wa elektroniki umetengenezwa kwa gharama ya sh. milioni 537 na kwa sasa wizi uliokuwa unafanywa na watumishi wasio waaminifu utapungua.