Thursday , 30th Apr , 2015

Baadhi ya askari polisi na maafisa wa idara mbalimbali za serikali wanaolinda katika vizuizi vya barabara kuu ya Mwanza-Tarime wanadaiwa kuomba na kupokea rushwa ili kuruhusu magari yanayobeba ng’ombe kwenda nchini Kenya.

Kaimu Kamanda wa polisi Kanda maalum ya tarime Kamishina msaidizi wa jeshi la polisi ACP Sweetbert Njewike.

Baadhi ya wasafirishaji wa ng’ombe hao wamedai kuwa licha ya kuwa na vibali kutoka idara ya mifugo na kulipia ushuru unaotakiwa lakini wamekuwa wakilazimishwa kutoa rushwa hiyo kwa kila kizuizi jambo ambalo limewafanya baadhi yao kupita maporini hadi nchini kenya ili kukwepa usumbufu huo.

Hata hivyo kaimu kamanda wa polisi kanda maalum ya tarimena Rorya kamishina msaidizi wa jeshi la polisi Sweetbert Njewike, amekiri jeshi hilo kupata malalamika hayo ya rushwa na kwamba yamekuwa yakifanyiwa kazi lakini amesema wasafirishaji hao pia wamekuwa wakikiuka sheria za nchi.

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ambaye pia ni mkuu wa wilaya ya Tarime Bw Glorious Luoga, amesema pamoja na viongozi mbalimbali wa serikali kuwahamasisha wafugaji kupunguza mifugo yao kwa kuuza, lakini wafanyabiashara wa ng’ombe licha ya kuwa na vibali kutoka mamlaka za serikali wamekuwa wakipata vikwazo katika kusafirisha mifugo hiyo hatua ambayo imewafanya sasa kulazimika kutoa rushwa katika vizuizi hivyo.