Jumanne , 24th Jan , 2017

Serikali imefuta rasmi utaratibu kwa wakimbizi kuingia nchini kwa makundi kutokana na baadhi yao kujihusisha na vitendo vya uhalifu hasa unyang'anyi wa kutumia silaha za moto.

Silaha zikiteketezwa

 

Agizo hilo limetolewa leo mjini Kigoma na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Mwigulu Nchemba, wakati akiongoza zoezi la kuteketeza silaha haramu 5, 608 zilizokamatwa kwenye matukio ya kihalifu na zingine kusalimishwa na wamiliki kwa vyombo vya usalama, tukio lililoratibiwa na Kituo cha Kikanda cha Kudhibiti Uzagaaji wa Silaha Katika Nchi za Maziwa Makuu na Pembe ya Afrika.

Mhe. Mwigulu amesema, katika kukabiliana na uzagaaji wa silaha haramu Tanzania imetia saini mikataba ya kimataifa na itifaki za kikanda za kufanya oparesheni maalum kwa kushirikiana na nchi jirani ya uwekaji alama maalum ya kutambua silaha hizo na kufanya marekebisho katika baadhi ya sheria kulingna na wakati.

Ameongeza kwamba, hivi sasa serikali inaangalia utratibu mpya wa kuweka silaha maalum za uwindaji kwa wale wanaopewa vitalu vya kuwinda kuwa na sehemu maalum ya kuchukua silaha na baada ya matumizi zinarudishwa sehemu husika ili kuhakikisha usalama kwa wanachi.