Ijumaa , 17th Jun , 2022

Uongozi wa klabu ya Simba umefikia makubaliano ya kumuuza kiungo mshambuliaji Rally Bwalya kwa timu ambayo hatutaiweka wazi kwa sasa kutokana na matakwa ya kimkataba.

Rally Bwalya

Bwalya atacheza mchezo wake wa mwisho Jumapili hii dhidi ya KMC na baada ya hapo ataruhusiwa kuondoka kwenda kujiunga na timu yake mpya ambayo inataraji kuanza maandalizi ya msimu  (Pre Season)  hivi karibuni

Kwa heshima ya mchezaji ambae amedumu nasi kwa misimu miwili tutautumia mchezo wa Jumapili dhidi ya KMC utakaofanyika Uwanja wa Benjamin Mkapa kumuaga rasmi nyota huyo raia wa Zambia

Bwalya alijunga nasi Agosti 2020 kutoka Power Dynamos ya Zambia kwa mkataba wa miaka mitatu ambapo mpaka anaenda kujiunga na timu mpya alikuwa amebakisha kandarasi ya mwaka mmoja.

Kwa misimu miwili aliyodumu nasi Bwalya ameisaidia Simba kushinda mataji matatu ikiwemo ligi kuu Tanzania Bara, Kombe la Shirikisho la Azam Sports, Kombe la Mapinduzi pamoja na ngao ya jamii

Bwalya pia ameisaidia Simba kufika robo fainali ya ligi ya mabingwa Afrika msimu wa 2020/2021 na Kombe la Shrikisho barani Afrika kwenye msimu wa 2021/2022.

Uongozi wa klabu ya Simba  unamtakia heri Rally Bwalya katika maisha yake mapya ya soka katika timu mpya.