Jumanne , 26th Jan , 2016

Aliyekuwa mlinzi wa Liverpool pamoja na timu ya taifa ya Ureno Abel Xavier ameteuliwa kuwa mkufunzi mpya wa timu ya taifa la Msumbiji.

Nyota wa zamani wa klabu ya Liverpool Abel Xavier enzi zake akicheza soka.

Xavier ambaye pia aliichezea Everton na timu ya LA Galaxy ya Marekani alizaliwa nchini Msumbiji lakini akiwa mtoto alielekea nchini Ureno na kulichezea taifa hilo kimataifa.

Kocha huyo mwenye umri wa miaka 43 amepewa mkataba wa miaka miwili na ataanza kazi yake tarehe mosi mwezi Februari.

Amepewa jukumu la kuisaidia 'the Mambas' ili kufuzu katika michuano ya kombe la bara Afrika mwaka 2017.

Msumbiji iko chini ya kundi H, baada ya kupoteza mechi zake zote mbili kufikia sasa, nyumbani dhidi ya Rwanda na baadaye ugenini nchini Mauritius.

Mechi yake ya kwanza itakuwa dhidi ya Ghana ambao ndio viongozi wa kundi hilo baada ya kushinda mechi zote mbili.