Jumapili , 18th Feb , 2018

Viongozi wa timu ya Toto Africans ya Mwanza ambayo imeshuka kutoka ligi daraja la kwanza hadi ligi daraja la pili wamedaiwa kuanza kuingia mitini na baadhi ya vifaa vya timu hiyo.

Mmoja wa viongozi wa timu hiyo amedai kuwa kuna viongozi ambao walisafiri na timu kwenda mjini Dodoma kwenye mchezo wa mwisho lakini hadi sasa hawajarejesha vifaa vya timu hiyo ikiwemo magodoro.

“Wapo viongozi ambao waliondoka na timu kwenda Dodoma kwenye mechi dhidi ya Dodoma FC na baadae Dar es salaam kucheza FA Cup na kuna baadhi ya vifaa walichukua kwa ajili ya kwenda navyo nasikia havijarudi kambini'', amesema.

Aidha kiongozi huyo ambaye hakutaka jina lake litajwe amesema wamepanga ikifika Jumatano mchana bado viongozi hao wasio na uchungu na timu hawajarudisha vifaa  watakwenda polisi kwa sababu itakuwa ni wizi kama wizi mwingine.

Toto ambayo iliwahi kushiriki ligi kuu soka Tanzania Bara na kushuka daraja msimu uliopita hadi daraja la kwanza imejikuta ikishindwa kurejea ligi kuu na kuziacha timu za Biashara Mara na Alliance Schools zikipanda ligi kuu.