Jumatatu , 8th Jun , 2015

Safari ya Timu ya Taifa ya mpira wa Netball Taifa Queens kushiriki mashindano ya Afrika yanayotarajiwa kufanyika nchini Namibia huenda ikaota mbawa kufuatia timu hiyo kukabiliwa na ukata.

Katika taarifa yake, Mwenyekiti wa Chama cha Netiboli nchini CHANETA Anna Kibira amesema, licha ya timu hiyo kuendelea na mazoezi kwa ajili ya kujiandaa na michuano hiyo lakini hawana uhakika wa kushiriki michuano hiyo kutokana na kutokujitokeza kwa wadhamini kwa ajili ya kuisaidia timu hiyo.

Kibira amesema, timu hiyo imeingia kambini kwa awamu ya pili ambapo inaendelea na mazoezi kwa ajili ya kujiandaa vyema na michuano hiyo inayotarajiwa kuanza kutimua vumbi Juni 28 mpaka Julai tano mwaka huu.

Kibira amesema, kikosi hicho kinachotarajiwa kuondoka kikiwa na wachezaji 12 chini ya kocha Nafsa Ibrahim kinatarajiwa kuondoka Juni 26 kwa ajili ya kushiriki michuano hiyo.