Ijumaa , 20th Sep , 2024

Uongozi wa klabu ya Simba, umesema kuwa timu hiyo ina mlima mkubwa Jumapili, Septemba 22 katika mchezo wa pili wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Al Ahly Tripoli ya Libya.

 

Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally amesema hayo katika uzinduzi wa hamasa kuelekea mchezo huo ambao Simba watakuwa nyumbani Uwanja wa Benjamin Mkapa Dar es Salaam.

“Jumapili tuna kibarua kigumu kwelikweli, Kila mwanasimba anatakiwa kutambua kuwa tuna mlima mkubwa sana, tusiichukulie poa kwa kuwa tunacheza nyumbani.

Tuna kazi kubwa na ngumu kuweza kufuzu kwenda kucheza makundi, mashabiki na wanachama wajitokeze uwanjani kwa wingi kurahisisha kazi ” amesema Ahmed.

Ameongeza kuwa wote waliona vijana walicheza kwa nidhamu Libya licha ya vurugu zote. Sasa ngoma inahamia nyumbani tunatakiwa kuwapa nguvu wachezaji kufuzu hatua ya makundi jambo la kila Mwanasimba.

“Mechi yetu ndio yenye mvuto zaidi Afrika wikiendi hii, sisi kama Mnyama hatutaki kuishia hatua hii kwa mapenzi yake Mwenyezi Mungu, tuna timu nzuri sana, pia viongozi tumejipanga kuhakikisha Simba yetu inafuzu makundi,” amesema Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Simba.

Ameongeza kuwa hawawezi kufuzu bila ya mashabiki wa Simba kuungana kwa pamoja na kuujaza Uwanja wa Mkapa, Al Ahly Tripol hana sehemu ya kutokea.

“Mechi ya kwanza pale Libya waliwafanyia sana vurugu wachezaji wetu tuliona vitendo vingi vya ovyo ambavyo walifanya lakini inabidi tuwe kinyume chao sababu ni timu kubwa Afrika lakini pia tumeshapewa Tuzo ya Mashabiki Bora Afrika, Kama unaweza kumuua adui yako kwa asali ya nini kutumia sumu?” Amesema Ahmed Ally.

Ameeleza kuwa hawajawahi kucheza hatua hii ya kutafuta kufuzu dhidi ya waarabu, ni mara ya kwanza mara zote wanakutana na UD Songo ya Msumbiji, Nkane ya Zambia nk.

“Hii ni mara yetu ya kwanza kucheza na waraabu kuingia kutafuta nafasi ya kufuzu makundi, kila mmoja wetu anahitaji hii nafasi kazi kubwa ni kwetu kuhakikisha tunafikia malengo yetu,” amesema meneja huyo.

Ameongeza kuwa wapinzani wao Al Ahly Tripoli wanaitaka hii mechi kwa sababu wamekuja kwa kuitaka hii mechi kwa kuwa wamekuja na kupewa walinzi.

“Licha ya kuja kukodi mabaunsa lakini haizuii mashabiki kujitokeza uwanjani kusapoti vijana wetu ili kuwapa nguvu kupambania na kufuzu hatua ya makundi.