Alhamisi , 12th Nov , 2015

Kamati ya utendaji ya Klabu ya Simba SC inatarajia kukutana siku yoyote kuanzia sasa kuweza kujadili mgogoro uliopo kati ya kocha mkuu wa klabu hiyo Dylan Kerr na msaidizi wake Suleiman Matola uliopelekea Matola kujiuzulu kuifundisha klabu hiyo.

Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa Klabu ya Simba Hajji Manara amesema, Matola alikutana na Rais wa Klabu hiyo Evance Aveva na kumueleza mgogoro uliopo dhidi ya Kerr ambapo alimueleza ameamua kujiuzulu na Rais Aveva alilipokea.

Manara amesema, kuhusiana na mgogoro uliopo kati ya makocha hao, kamati ya utendaji imedhamiria kukutana lakini makocha wote wawili pamoja na wanachama wanatakiwa kuwa watulivu huku wakisubiri kamati hiyo mpaka itakapokutana.

Kwa upande wake kocha Matola amesema, kutokuelewana na Kocha Kerr kunatokana na kocha huyo kuwa mbishi na kutokukubali ushauri kwa ajili ya manufaa ya timu hivyo yeye kama kocha msaidizi kaamua kumuachia timu ili aendelee nayo.

Matola amesema, alikuwa na matatizo na Kerr kabla ya ligi kusimama na hata katika ripoti yake Kerr alieleza kutokuelewana huko hivyo imebidi kumuachia ili aendelee na kazi ili kuweza kuinusuru timu.