Jumatano , 3rd Oct , 2018

Baada ya klabu ya Simba kumpitisha mfanyabiashara Mohammed Dewji kama mwekezaji kupitia mfumo wa hisa akimiliki asilimia 49 ya hisa, ameanza kutekeleza ahadi yake ya kujenga uwanja wa klabu.

Kulia ni mwekezaji wa Simba Mohammed Dewji

Mo Dewji amethibitisha kuanza kwa ujenzi wa uwanja wa mazoezi wa klabu hiyo uliopo katika eneo la Bunju jijini Dar es salaam. Tayari tingatinga lipo uwanjani hapo likiendelea kusawazisha eneo hilo ili ujenzi wa eneo la kuchezea (Pitch) uanze.

''Huu ni wakati wa kihistoria kwa klabu yetu. Kwa miaka mingi nimekuwa nikiota na sisi tuwe na uwanja wetu wa mazoezi, na ninafurahi sasa ninawezesha hii ndoto baada ya miaka 82 tangu kuanzishwa kwa klabu yetu ya Simba.'' ameandika Mo Dewji.

Aidha mwekezaji huyo wa Simba ameweka wazi kuwa ujenzi huo unatarajia kukamilika ifikapo mwezi Februari mwaka 2019.

Hii ni moja ya ahadi alizozitoa siku alipotangazwa kuwa mshindi wa zabuni ya kuwekeza kwenye klabuni hiyo. Pia aliahidi kuifanya Simba kuwa klabu ya kimataifa kwa kusajili wachezaji wenye viwango vinayoendana na ukubwa wa klabu pamoja na kocha mwenye uwezo mkubwa.

Zaidi tazama video hapo chini ikionesha shughuli ya kusawazisha ardhi ikiendelea.