Jumanne , 12th Apr , 2016

Uongozi wa Klabu ya Azam FC umesema wachezaji wao Farid Mussa na Himid Mao wamepata ruhusa katika vilabu walivyotakiwa wakafanye majaribio mpaka watakapomaliza mchezo wa marudiano dhidi ya Esperance ya nchini Tunisia.

Afisa habari wa Azam FC Jaffery Iddy Maganga amesema, hapo awali Farid Mussa na Himid Mao walitakiwa wasicheze mchezo wa marudiano ya Esperance kwani walitakiwa kuelekea nchini Ubelgiji mara moja kwa ajili ya majaribio lakini uongozi umechukua jukumu la kuomba ili kumaliza mchezo huo.

Maganga amesema, mara baada ya kumalizika kwa mchezo huo wachezaji hao watafanya taratibu zote na wataanza safari ya kuelekea nchini Ubelgiji kwa ajili ya majaribio.

Azam FC inatarajia kucheza mchezo wake wa marudiano wa hatua ya 16 Bora Kombe la Shirikisho dhidi ya Esperance Aprili 19 nchini Tunisia ambapo katika mchezo wa kwanza uliopigwa mwishoni mwa wiki iliyopita Uwanja wa Chamazi Azam FC ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 2-1.