Jumatatu , 31st Oct , 2016

Bondia wa ngumi za kulipwa nchini Thomas Mashali amefariki dunia usiku wa kuamkia leo akiwa njiani kupelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili baada ya kupigwa na watu wasiojulikana, maeneo ya Kimara Jijini Dar es salaam.

Marehemu Thomas Mashali, enzi za uhai wake

Akithibitisha taarifa hizo, Rais wa Organaizesheni ya ngumi za kulipwa nchini TPBO Yassin Abdallh “Ostadh” amesema mauti yamemkuta Mashali baada ya kupigwa na watu wasiojulikana na mwili wake kuokotwa na wasamaria wema maeneo ya Kimara.

“Ni Mashali amefariki akiwa njiani wa wakati anapelekwa Muhimbili kwa ajili ya matibabu mara baada ya kupigwa na watu wasiojulikana, ” amesema.

Akizungumza katika kipindi cha SUPAMIX mmoja wa marafiki wakubwa wa marehemu ambaye pia ni mwanafunzi wake, bondia Fransis Miyeyusho amesema, jana  walikuwa pamoja na Mashali katika kikao cha mabondia na baada ya hapo Mashali alimuaga kwamba anakwenda zake Kimara na kwa kuwa ilikuwa ni kawaida yake kwenda huko haikuwa na shaka kwake hivyo wakaagana.

Baada ya hapo akapata taarifa usiku kwamba Mashali amepigwa na watu aliokuwa anagombana  nao akapelekwa hospitali ya Palestina na baadaye hospitali ya Muhimbili ambapo alifariki dunia.

“Yawezekana watu hawakufahamu kama wanayempiga ni Mashali kwa kuwa rasta alizokuwa nazo alizinyoa hivyo ni vigumu kwa watu tena usiku kumfahamu pengine ndiyo maana yamemfika hayo” – Amesema Miyeyusho.

 

 

 

 

 

Francis Miyeyusho