Jumapili , 11th Feb , 2018

Mshambuliaji wa klabu ya Simba, John Bocco amechaguliwa kuwa mchezaji Bora wa mwezi Januari kwenye Ligi Kuu soka Tanzania Bara akimbwaga mchezaji mwenzake Emmanuel Okwi.

Bocco ambaye pia ni nahodha wa Simba amewashinda Okwi pamoja na Awesu Awesu wa Mwadui kutokana na uchambuzi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za VPL.

Bocco alitoa mchango mkubwa kwa Simba mwezi huo ikipata pointi tisa katika michezo mitatu iliyocheza na kuendelea kubaki kileleni mwa msimamo wa ligi, huku mshambuliaji huyo akifunga mabao matatu na kutoa pasi mbili za usaidizi wa mabao.

Mshambuliaji huyo aliyesajiliwa na Simba msimu huu amecheza dakika zote 270 za michezo mitatu ya Simba mwezi Januari huku akionesha kiwango kikubwa katika kila mchezo.

Wachezaji wengine ambao tayari wameshinda tuzo hiyo msimu huu ni Okwi (Agosti), Shafiq Batambuze (Septemba), Obrey Chirwa (Oktoba). Wengine ni Mudathir Yahya (Novemba), Habibu Kiyombo (Desemba).