Jumapili , 12th Aug , 2018

Muongozaji mkongwe wa video nchini Adam Juma na mdau wa mchezo wa Kikapu nchini, ametoa mtazamo wake kuhusu game 5 za fainali ya michuano ya Kikapu ya Sprite Bball Kings kati ya Flying Dribbllers dhidi ya Mchenga Bball Stars, akisema ni ngumu kutabiri.

Mchenga Bball Stars (kijani) kwenye game 3 ya nusu fainali dhidi ya Portland (nyeupe).

Adam Juma ambaye amekuwa akihudhuria mechi mbalimbali za michuano hiyo inayoandaliwa na East Africa Television LTD na kupewa nguvu na kinywaji cha Sprite, alieleza kuwa kiwango ambacho alikiona kwa mabingwa watetezi Mchenga pamoja na Flying Dribblers anaamini fainali itakuwa nzuri.

''Fainali itakuwa ngumu sana, nafikiri itakwenda hadi game 5 kutokana na ubora wa timu mbili zilizoingia, kwa wapenzi wa Kikapu tusikose tu uwanjani maana tutapata kile tunachohitaji kutoka kwa timu hizi mbili'', alisema.

Adam Juma

Game za fainali za michuano hiyo ambayo inampa bingwa nafasi ya kutunza kitita cha shilingi milioni 10, huku makamu bingwa akitunza milioni 3 na mchezaji bora (MVP) akitwaa milioni 2, zitaanza Jumamosi Agosti 18 kwenye uwanja wa taifa wa ndani.

Flying Dribblers ambao waliwatoa Team Kiza kwenye nusu fainali wanacheza fainali yao ya kwanza baada ya msimu uliopita kutolewa katika nusu fainali na timu ya Mchenga Bball Stars ambao wanatetea ubingwa wao.