Jumanne , 6th Aug , 2019

Mtoto wa dereva wa Mkuu wa Mkoa wa Mara, aliyefahamika kwa jina la Kasobi Shida (26), ambaye alilazwa katika Hospitali ya Mkoa Mara, baada ya kupata ajali wakati akiendesha gari ya RC Adam Malima amefariki dunia.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara Juma Ndaki amethibitisha kutokea kwa kifo hicho ambapo amesema,  kifo hicho kimetokea kwa sababu ajali aliyoipata ilikuwa ni mbaya hali iliyopelekea kijana huyo kupata majeraha ndani ya mwili wake.

''Ni kweli amefariki na sababu ya kifo chake, baada ya madaktari kumfanyia upasuaji waligundua utumbo wake umepasuka na damu imevujia ndani kwa ndani'' amesema RPC Ndaki.

Aidha Kamanda Ndaki akielezea hali ya Dereva wa Mkuu wa Mkoa (Baba wa Marehemu), amesema hali yake inaendelea vizuri na kwamba madaktari wanaendelea kumfanyia ushauri wa kisaikolojia ili arejee kwenye hali yake ya kawaida.

Kasobi Shida alipata ajali siku ya Agosti 4, baada ya kuchukua gari hilo bila ridhaa ya mzazi wake ambapo lilimshinda kuendesha na kutoka nje ya barabara kisha  kugonga daraja.