Jumatano , 11th Sep , 2024

Jeshi la Polisi nchini linawashikilia walimu wanne na mfanyabiashara mmoja kwa tuhuma za kuwatapeli wananchi kwa kuwadanganya kuwekeza katika sarafu za kimtandao (cryptocurrency) na matokeo yake kutoweka na fedha zao walizowekeza.

Msemaji wa Jeshi la Polisi DCP David Misime

Akizungumza leo Septemba 11, 2024 Msemaji wa Jeshi la Polisi DCP David Misime, amesema kuwa watuhumiwa hao walikamatwa katika hoteli ya Gold Crest Jijini Mwanza  kufuatia malalamiko ya wananachi kutapeliwa fedha zao.

"Baada ya kufungua makampuni hayo na kuwalaghai wananchi kuwekeza fedha huwa waliowekeza mwanzo hupewa fedha kiasi kuonesha fedha walizowekeza zimezaa faida ili kuwapa matumaini na kuendelea kuvutia wengine ili wajitokeze kuwekeza na wakishapata wawekezaji wengi na fedha kuwa nyingi hufunga kampuni hizo na kutoweka kabisa kwenye mtandao, waliowekeza wanapojaribu kufuatilia kampuni hizo wanashindwa kuwapata na kuwasiliana kama walivyokuwa wanawasiliana wakati wanahamasishwa kuwekeza na ndipo hubaini wamesha tapeli," amesema DCP Misime

Misime amewataka wananchi kuchukua tahadhari na kujiepusha na udanganyifu na ulaghai wa kitapeli kama huo kwani pamoja na kuwepo na teknolojia ya uwekezaji mtandaoni (cryptocurrency) bado teknolojia hiyo utaratibu wake haujaanza kutumika hapa nchini.