Jumatatu , 22nd Jul , 2024

Waziri Mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu ameelekea jijini Washington ambapo anatarajiwa kuhutubia bunge la Congress wakati mvutano ukionekana kuwepo kati ya mataifa hayo mawili kutokana na vita vya Gaza.

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu

Kwa mujibu wa Netanyahu ziara hii ni muhimu haswa wakati huu Washington ikionekana kuishinikiza Israel kuafikia muafaka wa kusitisha mapigano na Hamas.
Netanyahu atakuwa kiongozi wa kwanza kuhotubia mabunge yote mawili mara nne kwa pamoja nchini Marekani Winston Churchill wa Uingereza akiwa amefanya hivyo mara tatu.

Mpango uliokubaliwa mwezi Mei ulipendekeza kusitishwa kwa mapigano kwa wiki sita wakati baadhi ya mateka wa Israel wangebadilishwa na Wapalestina wanaoshikiliwa katika magereza ya Israel.

Israel imezidisha mashambulio yake dhidi ya Gaza katika wiki za hivi karibuni na Netanyahu amesisitiza kuwa kuzidisha shinikizo za kijeshi ndiyo njia pekee ya kuwakomboa mateka na kuwashinda Hamas.

Wakati hayo yakijiri Mawaziri wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya wamekutana leo Jumatatu Brussels kujadili migogoro inayoendelea nchini Ukraine na Mashariki ya Kati.