Jumanne , 24th Jan , 2023

Katekista wa kanisa la Roman Catholic parokia ya Mlangali wilayani Ludewa mkoani Njombe, Simon Njavike (43) amepandishwa kizimbani katika mahakama ya wilaya hiyo kwa kosa la kumbaka mwanafunzi wa kidato cha tatu(17)  ambaye jina lake limehifadhiwa.

Kanisa

Akisomewa shtaka hilo na Mwendasha Mashtaka Angelo Marco, mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya wilaya ya Ludewa Isaac Ayengo, imeelezwa kuwa mshtakiwa huyo ni mwalimu wa watoto wa kipaimara na binti huyo ni mmoja wa wanafunzi hao na amekuwa akifanya vizuri katika mafunzo hayo hivyo katekista huyo alimpa sh. 10,000 kama zawadi ya kufanya vizuri kwenye mafunzo hayo.

Amesema baada ya siku kadhaa mshtakiwa huyo alianza kumtaka kimapenzi lakini binti huyo alikataa ndipo akaanza kudai kurudishiwa shilingi 10,000 yake aliyokuwa amempa lakini binti alishindwa kuirudisha kutokana na kutokuwa nayo.

Ameongeza kuwa baada ya siku kadhaa mshtakiwa huyo alimuita binti nyuma ya kanisa majira ya mchana ambako kuna kamsitu na binti alipofika akamkamata kwa nguvu na kuingia nae katika msitu huo kisha akatimiza lengo lake hilo na kutokomea kusiko julikana.

Hata hivyo jeshi la polisi lilifanya jitihada za kumtafuta na baada ya siku kadhaa alikamatwa na kufikishwa mahakamani ambapo mshtakiwa huyo amekana shitaka hilo na kupelekea kesi hiyo kuahirishwa mpaka itakapo tajwa tena February 09 mwaka huu.