Ijumaa , 4th Oct , 2024

Watu wawili ambao ni mke na mume wamefariki dunia baada ya mume kudaiwa kumuua mkewe kisha naye kujiua katika Kijiji cha Njirii Halmashauri ya Itigi wilayani Manyoni Mkoani Singida huku chanzo kikidaiwa kuwa ni ugomvi wa kifamilia.

Imeelezwa kuwa marehemu Janeth Stephano(36) alikutwa kitandani akiwa amefariki majira ya saa 2:00 usiku wa kuamkia tarehe 03 Oktoba 2024 baada ya watoto wake kurudi nyumbani huku mumewe akiwa hayupo ndipo kesho yake siku ya Alhamisi baada ya kumtafuta wakamkuta umbali wa kilomita mbili akiwa amefariki na baada ya kuangaza wakakuta kopo la sumu  ambalo imesadikika alikunywa sumu hiyo mpaka kupoteza maisha.

Epson Petro ni mtoto wa marehemu amesema kuwa siku ya tukio baba yake alimwambia aende mtaani akatafute hela ya matumizi nyumbani ndipo ilipofika usiku huo baada ya wadogo zake kutangulia kurudi wakakuta mama yao akiwa kitandani amefariki na baba akiwa hayupo.

"Tulikuwa tunamalizia kujenga matungilizi pale na baba, tulivyomaliza kujenga matungilizi hayo mimi nikarudi ndani kuja kulala nikaamka mida ya saa moja nilipoamka mida ya saa moja nikaelekea mtaani na wakati naondoka hapa nyumbani tuliongea tu vizuri akaniambia hebu wewe nenda mtaani ukatafute hela ya matumizi ya kula nyumbani  hebu nenda mtaani ukajaribu kutafuta hela tupate hela ya kutumia, ndio kama hivyo nilivyoenda mtaani kurudi nimekuta tukio kama hili," amesema mtoto

Akizungumza kwa niyaba ya Mganga Mfawidhi wa hospitali ya Wilaya Manyoni  dkt.Maziku Fabian amesema kuwa asubuhi ya Oktoba 03 walipokea miili hiyo miwili ambapo baada ya uchunguzi hakuna mwili uliokuwa na majeraha isipokuwa mwili wa Janeth ndio ulikuwa na alama shingoni.