Ijumaa , 25th Mei , 2018

Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dkt. Magufuli imetoa zaidi ya shilingi bilioni nne kwa ajili ya Taasisi na Watafiti walioshinda maandiko ya miradi nane ya utafiti ambayo itaanza kufadhiliwa mwaka huu wa fedha.

Akizungumza kabla ya kukabidhi tuzo za hundi kwa Taasisi zilizoshinda fedha hizo Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amesema miradi yote iliyopata fedha ni ile ya ambayo ina malengo madhubuti ya kuimarisha uchumi wa viwanda hadi 2025.

"Kufadhiliwa kwa miradi hiyo nane kutaleta mchango mkubwa wa uzalishaji wa dawa nchini na kupunguza uagizwaji wa dawa kutoka nje, uboreshaji wa maabara za uhandishi jeni, kuongeza ushindani wa bidhaa, kuongeza uzalishaji wa mazao, uzalishaji wa mimea pamoja na kuchangia katika uanzishwaji wa viwanda", amesema Ndalichako.

Hata hivyo, Prof. Ndalichako amezitaka taasisi zilizopata fedha hizo kuzitumia kwa uadilifu na kwa malengo yaliyokusudiwa na siyo vinginevyo.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia, COSTECH Dkt. Amos Nungu amesema moja ya jukumu la tume hiyo ni kuratibu shughuli za sayansi na teknolojia kupitia ufadhili wa mirafi ya utafiti.