Jumatatu , 15th Jul , 2024

Serikali imesema ipo mbioni kuongeza mabasi ya mwendokasi 100 jijini Dar es salaam ili kupunguza adha ya usafiri huo inayoendelea katika maeneo mbalimbali

Kauli hiyo imetolewa na Msajili wa Hazina Nehemiah Mchechu wakati akizungumza na wanahabari

"Tunaona changamoto inayotokea kwasasa kwenye usafiri wa Mwendokasi na tunajua namna inavyochafua taswira ya Mwendokasi nchini, kwasasa serikali ina umiliki mkubwa kwenye kampuni ya UDART hivyo tayari tumeanza mpango wa kutatua changamoto zinazojitokeza kwenye usafiri huu tukishiriakiana na taasisi za fedha ikiwemo mabenki"

"Tumepanga kuongeza idadi ya mabasi ya Mwendokasi yapatayo 100 ambayo yatajikita kutoa huduma kwenye njia kuu kwanza, tunaamini yatasaidia kutatua changamoto iliyopo kwasasa pia tunahitaji kampuni nyingi zaidi za utoaji huduma kwa sababu ikiwepo kampuni moja kuna hatari yake ndio maana huduma inakuwa na changamoto hivyo tunajua changamoto hii inawakera watanzania lakini ndani ya miezi sita itakuwa tayari imetatuliwa kwa kiasi kikubwa"  Nehemiah Mchechu - Msajili wa Hazina

Katika hatua nyingine Msajili wa Hazina Nehemiah Mchechu amesema wakuu wa Taasisi na wenyeviti wa bodi kote nchini wanatarajia kukutana mwezi Agosti mwaka huu jijini Arusha ili kujadili maendeleo ya mashirika na taasisi za Umma kote nchini kikao ambacho kitafunguliwa na Rais wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan

Amesema lengo la kikao kazi hicho ni kuyachochea mashirika ya umma kutafuta fursa za uwekezaji nje ya nchini kwa manufaa ya umma wa watanzania na kuhakikisha kuwa mashirika na taasisi za Umma zinaendeshwa kwa ufanisi mkubwa

Ikumbukwe kuwa hivi karibu baadhi ya mashirika ya umma na taasisi yalifutwa na mengine kuunganishwa ikiwa ni sehemu ya kuweka mifumo mizuri ya mashirika hayo kufanya kazi ambapo amesema yapo pia mashirika ambayo iwapo hayataonekana kufanya vizuri yatafutwa au kuunganishwa na mengine kama ilivyotokea hapo awali