Jumatano , 29th Nov , 2017

Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangalla amesema wahalifu wanazidi kubuni mbinu mpya baada ya kubaini ubora wa mifumo ya kiintelijensia inayotumiwa na wizara yake kubaini uhalifu dhidi ya raslimali.

Waziri Kigwangalla amesema hayo baada ya operesheni kwa kutumia Intelijensia (intelligence-led operations) kufanikisha kukamatwa kwa Lori la kubeba mawe ya gypsum ambalo lilikwa limebeba mbao zilizopatikana kwa njia zisizo halali.

“Kadri tunavyozidi kuimarisha ulinzi wa raslimali za taifa ndivyo wahalifu nao wanavyobuni mbinu mpya za kufanikisha uhalifu wao. Lakini mbinu zetu za kuendesha operesheni kwa namna ya kutumia intelijensia (intelligence-led operations) inazaa matunda”, ameandika Kigwangalla kwenye Ukurasa wake wa 'Twitter'.

Ijumaa ya taraehe 26/11/2017 majira ya asubuhi Lori lenye namba za T862 BTZ na tela lenye namba T545 BLA, mali ya kampuni ya Swift Motors, likiendeshwa na Bw. Baraka Jackson lilikamatwa likiwa limebeba mbao huku zikiwa zimefichwa na mawe ya Gypsum, katika kituo cha ukaguzi wa mazao ya misitu cha Kiranjeranje wilaya ya Kilwa, mkoa wa Lindi.

Hata hivyo waziri Kigwangalla amesema mifumo ya kisasa ya  Kiintelijensia inayotumiwa na wizara yake inatuwezesha kukamata wahalifu wa raslimali na mazao ya misitu kwa ujumla.