Jumapili , 18th Feb , 2018

Kamanda wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es salaam Lazaro Mambosasa, ameelezea hatua walizochukua kama jeshi la polisi kwa askari alimpiga risasi mwanafunzi Akwiina na kumsababishia kifo, wakati wa vurugu za uchaguzi.

Akizungumza na mwandishi wa www.eatv.tv , Kamanda Mambosasa amesema wamewashilkilia askari polisi sita ambao walikuwa eneo la tukio, lakini mpaka sasa hawamjui nani alifyatua risasi.

“Hajulikani aliyempiga, sasa kama risasi zimepiga sita utajua ni ipi!!? Tumewazuia askari wote lakini huwezi kujua ni ipi, tunaendelea na upelelezi, aliyepigwa sio muandamanaji ameenda kupigwa pemebeni huko, yaani ameenda kupigwa mtu ambaye hahusiki wala hajui chochote, ndio maana hatujui”, amesema Kamanda Mambosasa.

Kamanda Mambosasa ameendelea kuelezea kwamba hata risasi iliyopigwa inaleta utata kwani risasi iliyopigwa juu haiwezi kupasua kichwa vile, hivyo wanaendelea kufanya uchunguzi kujua ilikuwaje na nani alihusika kupiga hiyo risasi.

“Hatujui risasi iliyompiga huyo, kwa sababu za polisi zilizopigwa juu, ikishuka inakuwa haina nguvu ya kupasua kichwa vile, haiwezi kupasua kichwa vile, kwanza imetoboa tundu la gari, ikaenda ikampiga ikamparaza na mwengine, lakini tunaendelea kuwahoji hawa walioshikiliwa, kwa sababu walikuwa zaidi ya 200 na kila mmoja alikuwa anarusha mawe, anarusha nini, you never know mtu pengine alikuwa na silaha akaenda akafyatua tu risasi ikaenda bila malengo ikaenda ikamgusa yule mama  ", amesema Kamanda Mambosasa.