Jumatatu , 19th Jul , 2021

Jeshi la Polisi mkoa wa Geita limesema chanzo cha matukio ya moto katika shule ya sekondari ya Geita yaliyotokea hivi karibuni ni ugomvi wa muda mrefu kati ya wanafunzi wa kutwa na bweni, ambapo wanafunzi wa kutwa wamedai wanafunzi wa bweni wamekuwa wakipendelewa na uongozi wa shule.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Geita Henry Mwaibambe

Kamanda wa Polisi mkoani humo Henry Mwaibambe, ameyasema hayo wakati akitoa taarifa ya uchunguzi wa matukio matatu ya moto yaliyotokea kwa kufululiza shuleni hapo kati ya Julai 5, 6 na 14 mwaka huu, na kudai kuwa wanafunzi wa kutwa wanadai kwamba wenzao wa bweni wamekuwa wakipendelewa hasa kwenye masuala ya chakula.

Kamanda Mwaibambe ameongeza kuwa mbali na matukio ya moto shuleni hapo, shule hiyo pia imekuwa na historia ya kuwa na wanafunzi watukutu, wavuta bangi na waharibifu.