Jumatatu , 7th Oct , 2024

Baba wa familia na mkazi wa barabara ya nne jijini Tanga Alii Bagidad (60) mwenye asili ya Kiasia ambaye mke wake pamoja na dada wa kazi walikutwa wamenyongwa pamoja na kutobolewa macho yao wiki iliyopita na yeye amekutwa amekufa baada ya mwili wake kuokotwa katika eneo la Nguvumali B.

Mwili wa mtu huyo umekutwa katika eneo hilo lenye pori ambapo mpaka sasa bado haijajulikana chanzo cha kifo chake. 

Mashuhuda wa tukio hilo wamesema waligundua tukio hilo baada ya kusikia harufu kali iliyokuwa ikitokea eneo ambalo amekutwa amekufa na hivyo kuwalazimu kujua ni kitu gani kilichopelekea harufu hiyo na ndipo walipokutana na mwili huo.

Mjumbe wa mtaa wa Nguvumali B  amesema ndani ya siku mbili mfululizo alikuwa akikutana na harufu hiyo akiamini ni mizoga ya wanyama ambayo imekuwa ikitupwa  na wafugaji. 

"Polisi walikuja wakaangalia wakawapigia simu ndugu zao wamekuja kuhakikisha kama kweli huu mwili ni wa ndugu yao wakakiri kuwa ni ndugu yao na ndipo taratibu nyingine zikaendelea kwa ajili ya kuuhifadhi mwili huo," amesema mjumbe huyo wa serikali ya mtaa.

Katika taarifa ya awali jeshi la polisi lilimuhusisha marehemu na kifo cha mke wake pamoja na mfanyakazi waliokutwa wamenyongwa na kutobolewa macho nyumbani kwao barabara ya nne jijini Tanga.